WAZIRI wa Kilimo Hussein Bashe ametoa siku 14 kupatiwa gharama za uzalishaji na uchakataji wa zao la chai nchini.

Waziri wa Kilimo, Mh. Mohamed Hussein Bashe, ameitaka Bodi ya Chai Tanzania (TTB) kukaa na wadaa kutengeneza timu ya ufundi ili kutengeneza gharama za uzalishaji za mkulima na za kiwanda I'll kujua gharama halisi ikiwa ni kwa ajili ya kuboresha tasnia hiyo.
"Natoa maagizo kwa bodi ya chai kuunda timu maalum kwa ajili ya kusaidia wakulima na viwanda kushughulikia uwazi katika uzalishaji wa zao la chai hali ambayo itaongeza tija. Ndani ya siku 14 niwe nimepata taarifa ya gharama za uzalishaji,"alisema.
Amesema serikali imeweka mikakati ikiwemo kuongeza thamani ya zao la chai nchini kwa kuhamasisha uuzaji wa chai iliyochakatwa badala ya malighafi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwawezesha wakulima kunufaika zaidi kupitia vyama vyao vya ushirika.
Amesema Bodi ya Chai imenunua mashine tatu kati ya saba zilizopangwa kununuliwa mwaka huu wa fedha, hatua itakayosaidia kukabiliana na changamoto ya soko kufuatia kufungwa kwa viwanda vya Mohamed Enterprises Ltd (MeTL) na Marvella.
“Kama hatua ya mwanzo, mashine mbili ya kuchakata na ya kuchanganya chai zitafungwa katika eneo la Dindira, Korogwe na kukabidhiwa kwa wakulima wadogo kupitia AMCOS kwa makubaliano maalum na Bodi ya Chai,” amesema
“Chai yetu imekuwa ikiuzwa na mataifa mengine bila kufahamika kuwa ni ya Tanzania. Kupitia chapa yetu, sasa chai yetu itatambulika popote inapouzwa,” alisema.
Pia alisema Serikali kupitia Bodi hiyo imefanikiwa kufungua masoko ya chai katika nchi za Oman, Qatar, Dubai, Japan huku Wawekezaji kutoka China wakiwa wameshawasili hapa nchini